 |
| Ssenkoom kushoto akizungumza na mwandishi Uwanja wa Ndege Dar es Salaam jana usiku |
BEKI
mpya wa Simba SC, Robert Ssenkoom amesema kwamba anataka kuitumia klabu
hiyo kama daraja la kupandia kwenda Ulaya kucheza soka ya kulipwa.
Akizungumza
na mwandishi baada ya kuwasili Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius
Nyerere, Dar es Salaam usiku wa jana, Ssenkoom anayetokea URA ya kwao,
Uganda alisema kwamba kiu yake ni kucheza Ulaya.
Beki
huyo mwenye mwili sawa na beki mwingine aliyehama Simba kujiunga na
watani wa jadi, Yanga SC msimu huu, Kevin Yondan, alisema anaamini timu
yake mpya itamsaidia kutimiza ndoto zake hizo.
Alisema
anaifahamu Simba SC kwa kuwa mwaka jana alikuja nchini katika Klabu
Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame akiwa na URA na
akavutiwa nayo kwa ujumla.
“Ina
mashabiki wazuri, wanajua kuwasapoti wachezaji wao. Nataka niwe beki
bora hapa Tanzania, nina matumaini ya kufanya vizuri na ninawaahidi
mambo mazuri tu wapenzi wa Simba SC,”alisema.
Ssenkoom
ambaye amesaini Mkataba wa miaka miwili Simba SC amesema wapenzi wa
klabu hiyo watarajie kumuona anaanza mazoezi mara tu atakapokabidhiwa
vifaa vya mazoezi.
Beki huyo alitua majira ya saa 6 usiku wa jana Dar es Salaam na kulakiwa na viongozi na wapenzi wachache wa timu hiyo.
Anakuwa
Mganda wa tatu katika kikosi cha Simba, baada ya kipa Abbel Dhaira na
kiungo Mussa Mudde na kama Wekundu hao wa Msimbazi watafanikiwa
kumsajili Moses Oloya basi atakuwa anacheza timu moja ndugu zake watatu.
Kocha
Msaidizi wa Simba SC, Moses Basena pia anatokea Uganda na ndiye
aliyefanikisha usajili wa beki huyo na anashughulikia pia mipango ya
Oloya kutua Msimbazi.
Simba SC imekuwa ikihaha kuimarisha safu yake ya ulinzi tangu impoteze beki Kevin Yondan aliyenyakuliwa na watani, Yanga SC.
Mwanzoni
mwa msimu ilimsajili Lino Masombo kutoka DRC, ikamtema, baadaye
ikamsajili Mbuyu Twite kutoka Rwanda, lakini Yanga pia wakaingilia na
kumbadili mawazo akageuza njia kwenda Jangwani alipo sasa.
Ikamsajili
Paschal Ochieng kutoka Kenya, lakini haikuridhika naye ikamtema.
Ikamsajili Komabil Keita naye pia haikuridhika naye ikamtema na katika
mechi za mwishoni za msimu ikalazimika kuwapanga pamoja katika beki ya
kati, Shomary Kapombe na Mudde, ambao kidogo walipunguza matatizo.
Baada
ya kutua kwa Ssenkoom, sasa kocha mpya wa Simba SC, Alhaj Abdallah
Athumani Seif ‘King Kibadeni’ atakuwa na jukumu la kumtafutia mtu sahihi
wa kucheza naye pale katikati, kama atakuwa Kapombe ama Mudde au
yeyote, ili mradi kutengeneza ukuta imara.